Monday, 13 March 2017

KILIMO CHA VIAZI MVIRINGO .KINAENDELEA.

MAGONJWA YA VIAZI MVIRINGO
UTANGULIZI:
Maana:
Ugonjwa ni hali ambayo hutokea baada ya sehemu mojawapo ya mmea kushambuliwa na vijidudu au vimelea visababishavyo ugonjwa, hali ambyo husababisha kudhoofika kwa mmea na kushindwa kufanya au kuota vizuri. Kwa kawaida magojwa hayo husababishwa na vijidudu au vimelea kutoka kwa Fangasi, bakteria na virusi,au minyoo fundo ambayo ni viumbe ndogo zaidi visivyoweza kuonekana hata kwa jicho.

AINA ZA VIMELEA/VIJIDUDU

Fangasi – Hawa ni vimelea kwa sura vinaonekana kana nyuzu nyuzi ambazo huzaliana kwa kutoa unga unga (spores). Vijidudu hivi vinaweza
kuingia kwenye mimea kikamilifu kupitia vidonda, mashimo ya asili katika mimea, kubebwa na wadudu, au kuingia moja kwa moja wakati wa kupanda. Magonjwa yasababishwayo na vimelea hivi yanaweza kuenea kwa njia ya maji, udongo, upepo na mbegu na juu ya zana za kilimo. Mfano wa ugonjwa unaosababishwa na fangasi kwenye viazi ni ugonjwa wa ukungu au baka jani chelewa.

Bakteria – Hivi ni vimelea vidogo vidogo kuliko fangasi, vina uwezo wa kuzaliana kwa spores na kugawanyika vyenyewe. Huzaliana sana hasi vinapokuwa kwenye hali nzuri na mazingira mazuri ya kuzaliana. Bakteria huingia ndani ya mimea kupitia vidonda na mashimo ya asili au kusafirishwa na wadudu. Magonjwa yanayosababishwa na bacteria hasa kwa viazi ni mnyauko bakteria na kuoza kwa viazi vyenyewe.

Virusi - Virusi ni vijidudu/vimelea vidogo sana kuliko hata fangasi na bakteria. Hivi vimelea Haviwezi kuishi kwa kujitegemea lazima pawepo na kiumbe hai hasa mmea unaoruhusu kirusi kuishi na kuweza kuzaliana kwa wingi.
Virusi huenea kutoka mmea mmoja na mwingine kwa njia ya kupanda mbegu zilizokwisha ambukizwa, au na wadudu kama vile wadudu mafuta na nzi weupe.

Viwavi (Nematodes) - Viwavi ni vijidudu umbo kama minyoo midogo midogo. Minyoo hii huathiri mimea na kusababisha mmea kufa. Viwavi vinaweza kuenea kikamilifu na kwa haraka kwa njia ya udongo, maji na upepo, au zana za kilimo pembejeo na mbegu.

Magonjwa yote ni vigumu zaidi kuweza kuyatambua au kuyachunguza kuliko wadudu ndani ya mimea, hii ni kutokana mara nyingi magonjwa mengi hayaonekani kwa macho ya kawaida. Kwa mkulima kuweza kutambua kwamba kuna ugonjwa ndani ya shamba, ni mpaka aone dalili Fulani tofauti kwenye mmea ambazo si za kawaida.

Jinsi ya kupambana na magonjwa ya mimea

Kanuni za kujikinga na magonjwa

Kwa kawaida ili ugonjwa uweze kutokea na kushambulia mimea shambani, ni lazima pawepo na vitu vitatu. Vitu hivyo ni Vijidudu/vimelea vya kusababisha ugonjwa, hali au mazingira yanayoruhusu kustawi kwa vimelea hao, pamoja na mmea wenyewe. Mambo haya matatu yanahusiana na kutegemeana kila mmoja na mwenzake.


Yakufanya ili ugonjwa usizuke na kushambulia mimea ni kama yafuatayo:-
1.      Kuzuia chanzo cha vimelea.
     •   Kufanya usafi wa mazingira
·         Kuharibu mabaki ya mimea inayowezi kuambukiza ugonjwa
·         Kuchagua mashamba yasiyo na historia ya magonjwa
·         Kama ni kilimo cha umwagiliaji, tumia maji safi kwa ajili ya umwagiliaji na
·         Kutumia mbegu za viazi zisizokuwa na magonjwa
·         Kutumia kilimo mzunguko wa mazao.

2.      Kutumia mmea husika:
·         Kwa kutumia mbegu za viazi zilizo safi na bora zenye ukinzani wa magonjwa mbalimbali.
·         Matumizi ya viwango sahihi vya mbolea.
·         Kupanda kwa majira sahihi ili kuepukana na milipuko ya magonjwa

3.      Sambamba na mabadiliko ya hali ya mazingira:
·         Kupanda viazi mwishoni mwa msimu wa mvua au mwishoni mwa msimu wa ukame.

Kudhibiti kwa kutumia viumbe hai

Kama ilivyo kwa wadudu, magonjwa pia yana maadui wanaozuia magojwa au vimelea vya magonjwa visiweze kustawi. Vimelea au bacteria wanaopatikana kwenye udongo wanaweza pia kutumika kwa ajili ya kuzuia magonjwa mbalimbali ya mimea. Mkulima anashauriwa kutumia mbolea asili ili kuweza kuongeza wingi wa viumbe hai kwenye udongo. Baadhi ya vimelea hutengenezwa na kuuzwa kwa ajili ya kutokomeza vimelea wengine ndani ya udong. Kwa mfano adui Kuvu Trichoderma ambaye ni Kuvu husaidia hupunguza fangasi nyingine wanaotokana na udongo.

Kudhibiti kwa kutumia kemikali za viwandani

Katika kilimo cha viazi mviringo, bado ni vigumu kuondoa matumizi ya madawa ya kuulia wadudu na kuzuia magonjwa. Hii inatokana na kuongezeka kwa vimelea vya magonjwa na wadudu shambani kwa sababu ya mabadiliko ya tabia nchi. Wakulima wengi wa viazi mviringo hutumia sana dawa za kuzuia ugonjwa wa ukungu, lakini jinsi ya kutumia na wakati gani pamoja na aina gani ya kiua kuvu kitumike, bado ni tatizo  kwa baadhi ya wakulima kama siyo wote. Tabia hiyo husababisha upinzani kwa vimelea wa ugonjwa husika, pia na mabaki ya madawa kusababisha sumu ndani ya viazi na kwa mazingira kuharibika. Kwa sababu hiyo, mbinu bora ya udhibiti wa magonjwa ni muhimu.

MAGONJWA MUHIMU YANAYOSUMBUA KWENYE VIAZI MVIRINGO

Magonjwa yanayosababishwa na vimelea bacteria

1.      Mnyauko bakteria (Bacterial wilt)

Ni ugonjwa unaosababishwa na kimelea kiitwacho kwa lugha ya kitaalam Ralstonia solanacearum. Kimelea hiki hushambulia si tu viazi mviringo bali hata na mimea yote jamii ya viazi kama vile pilipili, nyanya, tumbaku na bilinganya, Ugonjwa huu ni hatari sana, hasa katika maeneo ambako viazi mviringo vinalimwa. Ugonjwa huu hupunguza kiasi cha mavuno ya viazi mviringo hata kufikia asilimia 90, Wakulima wengi hutumia madawa ya kuzuia ukungu ili kudhibiti ugonjwa huu bila mafanikio kwani ugonjwa huu hautibiwi kwa dawa yoyote.

DALILI ZA UGONJWA WA MNYAUKO BACTERIA
Dalili za maambukizi ya ugonjwa wa mnyauko bakteria zinaweza kuonekana sehemu ya juu ya mimea ulioambukizwa. Dalili huanza kuonekana kwenye incha za majani kisha mmea huanza kunyauka wote au baadhi ya mashina. Dalili nyingine hujitokeza kwenye mizizi na mashina, ambapo mkulima anaweza kuzitambua kwa kukata shina na kuangalia ndani ataona michiriizi ya rangi ya kahawia. Kama ikitokea mmea ukawa na viazi tayari, basi mkulima anaweza kuona majimaji yanatoka kwenye macho ya kiazi, hali hii husababisha udongo kugandamana kwenye macho ya kiazi, hata hivyo mkulima anaweza kudhibitisha kwa kukikata kiazi na kukiangalia kwa ndani ataona michirizi ya rangi ya kawia. Hii inatosha kumwonesha mkulima kuwa viazi vyake au shamba lake lina ugonjwa wa mnyauko bakteria. Kiazi kilichaambukizwa na ugonjwa pia huonesha dalili za kuoza.
Njia nyingina ambayo anaweza kuitumia mkulima, ni kuchukua glasi iliyojaa maji masafi, kisha kukata kipande cha shina la mmea ulioambukizwa na kukining’iniza ndani ya maji, ataona ute mweupe unashuka ndani ya maji kutoka kwenye lile shina.

Nini chanzo cha kuenea kwa ugonjwa huu?
Mimea ya viazi mviringo huweza kupata maambukizi ya ugonjwa wa myauko bacteria kutoka kwenye;-
1.      Udongo – Vimelea vya ugonjwa huweza kuishi ardhini kwa muda mrefu.
2.      Maji ya mvua au kumwagilia
3.      Mbegu zilizo athrika tayari
4.      Magugu yatunzayo vimelea vya ugonjwa
5.      Mabaki ya viazi au mimea ya viazi mviringo
6.      Zana za kilimo zitumikazo shambani na mifugo

JINSI YA KUDHIBITI UGONJWA WA MNYAUKO BAKTERIA
Ugonjwa wa mnyauko bacteria hauwezi kudhibitiwa na madawa ya kuzuia ukungu kama wakulima wengi wanadhani. Dawa halisi ya kudhibiti ugonjwa huu haipo sana madukani, n ahata hivyo dawa ikipatikana huuzwa ghali, kiasi cha kumfanya mkulima kushindwa kumudu. Kimsingi ugonjwa wa mnyauko bacteria unaweza kudhibitiwa kwa kufanya haya yafuatayo:-
1.      Kupanda viazi mviringo kwenye shamba lisilokuwa na vimelea vya ugonjwa.
2.      Kutumia mbegu safi zisizokuwa na ugonjwa hasa mkulima anashauriwa kununua mbegu kutoka kwa wazalishaji wataalam wa mbegu za viazi mviringo.
3.      Kutumia kilimo cha mazao mzunguko na mazao mengine yasiyo ya jamii ya viazi. Kwa mfano;- Mazoezi mazuri ni mzunguko wa  viazi na mahindi au ngano au carrot.
4.      Kuondoa mabaki ya viazi na mimea ya viazi mara tu baada ya kuvuna.
5.      Kusafisha zana za kilimo baada ya kutumia.

2.      Upele upele mweusi (Common scab)
Huu ni ugonjwa unaosababishwa na fangasi aitwaye kwa jina la kitaalam kama Streptomyces scabies, ni maarufu kwenye udongo wenye tindikali ndogo (low pH). Ugonjwa huu hauna madhala makubwa kwa upande wa mavuno ya viazi, hata hivyo, unaathiri muonekano wa viazi vyenyewe, na hivyo kupunguza ubora. Kwa wazalishaji wa mbegu ni vema wakajua namna ya kukabiliana na ugonjwa huu, kwani unasababisha kupungua kwa ubora wa mbegu, kisha kupunguza hata bei ya kuuzia.Pia  huathiri hata kwa wauzaji wa viazi vya kusindika viwandani na wale wanao safirisha nje ya nchi.
DALILI ZA UGONJWA WA MAPELE MEUSI
Dalili zake huonekana kwenye kiazi chenyewe, viazi hupasuka ngozi, na mwishowe kuwa na madoa meusi kwenye ngozi ya kiazi.

Chanzo cha maambukizi
Ugonjwa huu unaweza kuambukizwa kutoka kwenye udongo, mbolea aina ya mboji au mbegu za viazi zilizoathrika tayari au maji yanayotumika kwa kumwagilia.

Jinsi ya kudhibiti Ugonjwa
Unaweza kudhibiti ugonjwa wa mapele kwa kufanya yafuatayo:
1.      Kuepuka kupanda katika mashamba yenye tindikali kidogo, au kwa udongo wenye tindikali kidogo, mkulima anashauliwa kuongeza madini ya chokaa.
2.      Kwa kutumia mbegu iliyo safi na bora.
3.      Kutumia mazao mzunguko
4.      Kutokomeza kabisa mabaki ya mimie ndani ya shamba lililoathirika.

3.      Ugonjwa wa ukungu au Kuvu (Late blight)
Huu ni ugonjwa muhimu Zaidi kwa wakulima wa viazi mviringo. Ugonjwa huu husababishwa na fangasi aina ya Phytophthora infestans, na kuathiri mazao ya viazi mviringo katika Nyanda za kitropiki. Mara kwa mara husababisha kudhoofika kwa mazao shambani, mimea hupata ugonjwa huu mara tu baada ya kuota mpaka wakati wa mavuno. Maambukizi mengi hutokea katika nyakati za mvua kubwa, unyevunyevu mwingi na na kipindi cha baridi kali. Wakulima wengi hutumia viua kuvu kwa ajili ya kudhibiti ugonjwa huo.

Dalili za ugonjwa wa Ukungu
Dalili za ugonjwa huu hutokea hasa kwenye majani, shina na kwenye viazi vyenyewe. Majani yaliyoathirika huonekana kama yaliyochubuka au kama yaliyowekwa kwenye maji ya moto. Hali hii hupelekea majani hayo kuoza na kukauka. Wakati maambukizi bado ni hai, unga mweupe huonekana chini ya majani, na mashina yaliyoambukizwa huanza kuoza kuanzia juu kwenye teke teke, na hatimaye kukauka. Viazi vilivyathrika na ugonjwa wa ukungu huonesha rangi ya kawia kwenye ngozi. Maambukizi yakiwa makubwa sana, na dawa ya kudhibiti ikicheleweshwa, mazao yaweza kuharibika ndani ya siku mbili au tatu.

Chanzo cha maambukizi
Ugonjwa wa ukungu unaweza kuambukizwa kwa njia ya hewa, udongo, maji, mbegu na mabaki ya mimea iliyoambukizwa. Huenea kwa haraka sana kupitia njia ya hewa, udongo, maji na mbegu zilizoathrika. Poda nyeupe juu ya uso wa majani yalioathirika inaweza kubebwa na upepo na kueneza ugonjwa kwa mimea mingine.

Jinsi ya kudhibiti ugonjwa wa Ukungu
Mambo muhimu ya kuzingatia ili kuweza kudhibiti ugonjwa huu ni kufanya haya yafuatayo;-
(1) Matumizi ya mbegu za viazi zenye ukinzani
(2) Kufanya uchunguzi wa shamba mara kwa mara ili kugundua ugonjwa kama upo
(3) Kutumia Mbegu safi isiyo na ugonjwa
(4) Kutumia kilimo mzunguko wa mazao.
(5) Kupanda mbegu za muda mfupi
(6) Kukata majani ya viazi siku 90 baada ya kupanda
(7) Matumizi ya madawa ya kuzuia na kutibu ukungu. Mkulima anashauriwa kutumia madawa ya kuzuia ukungu kama vile farmerzeb au sunstar au ridomil. Iwapo ugonjwa utaonekana tayari shambani, basi anaweza kutumia dawa kama Linkomil au Ridomil yenye kiambatanisho cha metalaxiyl. Dozi iliyopendekeza kwa dawa za ukungu ni 2.5 g ya dawa kwenye lita moja ya maji.

VIRUSI VYA VIAZI MVIRINGO
Kama ilivyo kwisha elezewa hapo mwanzo, Virusi ni vijidudu/vimelea vidogo sana kuliko hata fangasi na bakteria. Hivi vimelea Haviwezi kuishi kwa kujitegemea lazima pawepo na kiumbe hai hasa mmea unaoruhusu kirusi kuishi na kuweza kuzaliana kwa wingi. Wao wanahitaji kuishi ndani ya mimea ili kukamilisha maambukizi mzunguko wao. Kwa wakulima wa viazi, ugonjwa wa virusi ni hatari sana kwani mara unapokuwa ndani ya mbegu za viazi, magonjwa yasababishayo na virusi hupunguza mavuno kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Virusi hivi huishi ndani ya mbegu za viazi mviringo na hali hiyo hupelekea mbegu kuota kwa shinda hata kupunguza mavuno. Virusi vinapokuwa ndani ya mbegu dalili zake huwa ni vigumu kwa mkulima kuzitambua
Ni vigumu kwa wakulima kupata uelewa wa magonjwa ya virusi kwa sababu:
• vimelea hivyo ni vidogo sana na siyo rahisi kuviona kwa macho.
• Maambukizi ya virusi ni nadra kusababisha mimea kufa. Dalili za wazi, kama mimea imeambukizwa na virusi, ni mabadiliko katika mwonekano wa mimea shambani. Hali hii hupelekea mavuno ya viazi kuwa na viazi vyembamba. Wakulima wengi wakati wa kuandaa mbegu za msimu unaofuata, huchagua mbegu ndogo ndogo, hivyo hata huzaaji wake huwa dhaifu kwani tayari zinakuwa zimebeba virusi.
Kuna aina kama sita za virusi wa viazi waliokwisha tambuliwa kwa hapa Tanzania. Aina hizo hutoa dalili zinazofanana, hata kupelekea ugumu wa utambuzi ni aina gani ya kirusi. Aina hizo ni;-
• Kirusi cha leafroll virusi (PLRV)
• Kirusi cha S (PVS)
• Kirusi cha X (PVX)
• Kirusi cha Y (PVY)
• Kirusi cha M (PVM)
• Kirusi cha A (PVA)

Jinsi ya kudhibiti magonjwa ya virusi:
• Kwa kutumia mbegu zilizosafi na bora. Ni hatari sana kwa mkulima kuendelea kuchagua viazi vya mbegu kulingana na ukubwa peke yake, mara nyingi mimea aliyoambukizwa na magonjwa ya virusi kwa ujumla huzalisha viazi vya saizi ndogo ndogo.

• Kung’oa na kutaketaza mimea yote aliyoambukizwa na magonjwa ya virusi: Kwa wakulima wazalishaji wa mbegu, wanashauriwa kuchunguza mashamba yao, na kuhakikisha wanaondoa na kuteketeza mimea yote inayoonesha dalili za magonjwa ya virusi. Hii husaidia kwani virusi vingine husambaa kwa njia ya wadudu kama vila wadudu mafuta.

• Kudhibiti wadudu ambayo wanaweza kueneza magonjwa ya virusi: Kwa ujumla, wadudu kama vile wadudu mafuta, thrips, na inzi weupe.

• Kwa kutumia mbegu za viazi zenye ukinzania wa magonjwa ya virusi.

KUMBUKA: Virusi haviwezi kudhibitiwa na aina yoyote ya madawa ya kuulia wadudu.
Virusi aina ya Leafroll (PLRV)
Ugonjwa huu ni muhimu katika mimea viazi mviringo, na unaweza kusababisha mavuno kupunguzwa hadi kufikia 80%.

DALILI
Majani kujikunja kwa kwenda juu na kugeuka rangi ya njano. Kama ukiyagusa huwa yanatoa sauti kama majani yaliyokauka, kisha huwa yanavunjika vunjika. Maambukizi yakizidi husababisha mimea ya viazi huzaa viazi vidogo vidogo, au kutotoa viazi vyovyote.
Jinsi ugonjwa unavyoambukizwa

Virusi hivi vinaweza kuletwa ndani ya viazi au shambani na viazi vya mbegu vilivyoambukizwa au kwa kutumia wadudu mafuta ambao hueneza ugonjwa kutoka shamba moja hadi jingine.

Virusi aina ya PVY
Aina hii ni ya pili kwa umuhimu. Ni ugonjwa unaoweza kuambukizwa kupitia mbegu zilizoathrika au kwa njia ya wadudu mafuta na virusi hawa wanaweza kupunguza mavuno kwa 90%.

DALILI ZA UGONJWA
Majani ya mimea hukauka na kupasukapasuka, pia michirizi ya majani huwa ya rangi ya manjano.

Jinsi ugonjwa unavyoambukizwa
Japo kuwa ugonja huu unaweza kuambukizwa kutoka kwenye mbegu zilizoathrika na baadhi ya zana za kilimo zitumikazo shambani, pia ugonjwa huu unaambukizwa sana na wadudu mafuta ambao huweza kufyoza vimelea vya ugonjwa kutoka mmea mmoja na kupeleka mmea mwingine ndani ya muda mfupi.

Ugonjwa wa Minyoo fundo au Viwavi (Root-knot nematode)
Huu ni ugonjwa ambao huharibu sana sehemu za chini ya mimea, hasa viazi vyenyewe pamoja na mizizi ya viazi. Ingawa ugonjwa huu unapatikana katika maeneo mengi yanayolimwa viazi, lakini wakulima huona kama sio ugonjwa wa kutisha, hivyo kutoudhibiti.
Hata hivyo, viwavi hawa wanaweza kupunguza ubora wa mbegu kwa wakulima wanaojishughulisha na ulimaji wa mbegu za viazi mviringo. Vidonda vinavyosababishwa na viwavi hawa huweza kutoa mwanya wa maambukizi ya magonjwa mengine, hata kupelekea viazi kuanza kuoza.

DALILI ZA UGONJWA
Magonjwa yanayosababishwa na viwavi hawa hutofautiana, lakini dalili za kawaida za minyoo fundo ni:
• Kuvimba kwa viazi, na viwavi hao husababisha kiazi kuwa na maupele yenye kutoa maji maji endapo vikiminywa na kidole.

Jinsi ugonjwa unavyoambukizwa
Vyanzo vya magonjwa haya ni kupitia udongo uliokwishaathirika na mbegu zilizo na viwavi tayari. Viwavi vinaweza kuzunguka katika udongo kwa msaada wa maji.

Jinsi ya kudhibiti ugonjwa
Viwavi vinaweza kudhibitiwa kwa kufanya yafuatayo:
• Kwa kutumia mbegu zisizokuwa na ugonjwa.
• Kutumia kilimo mzunguko wa mazao kwa mfano mahindi au mazao mengine yasiyo jamii ya viazi.
• Kupulizia dawa maalum ya kuuwa viwavi ndani ya udongo

UPUNGUFU WA MADINI
Ishara ya ukosefu wa virutubisho ni:
• Nitrogen: 
1.      Njano njano ya majani.
2.      Kudumaa ukuaji wa mimea.

• Phosphorus:
1.      Mimea kuwa mifupi
2.      Majani kugeuka rangi ya kijani na kujikunja kwa kwenda juu.

·         Potassium:
1.      Mimea kudumaa, majani kuonekana meusi.

• Calcium:
1.      Mashina kukausha

2.      Majani madogo kujikunja.

No comments:

Post a Comment