UFUGAJI WA SAMAKI
UTANGULIZI
Ufugaji wa samaki unahusisha
kuwafuga samaki katika mazingira tengefu (yasiyo ya asili kwenye mabwawa au
matangi) na kuwavuna kwa aajili ya kula katika familia au kuwauza sokoni.
Historia ya ufugaji
wa viumbe-maji
inaonekana kuwepo tangu enzi za zamani sana. Katika maandishi ya mkono
yaliyoandikwa na Wachina wa kale karne ya 5 kabla ya Kristo yanaonyesha kuwa
Wachina walikuwa wanafuga samaki. Historia pia inaonyesha kuwa ufugaji mkubwa
ulijaribiwa na Wamisri wakati wa Ufalme wa kati (2052-1786 kabla ya Kristo) japo
hauonyeshi kama walifanikiwa na ufugaji huo. Ufugaji aina ya Kombe ulifuatiwa
na Warumi ambao kumbukumbu zake ziliwekwa vizuri na umeendelezwa katika njia
tofauti hata katika nyakati za sasa.Njia nyingi za ufugaji wa samaki za zamani
inatofautiana sana na njia tunazoziona leo hii na tofauti kubwa ni kwamba
zamani waliwavua samaki wadogo toka mazingira asili na kuwahamishia katika
mazingira yaliyotengenezwa kwa kufugia.
Ufugaji wa huu wa kisasa ulianza
kutumiwa mnamo mwaka 1733 pale ambapo mkulima wa Kijermani alipofanikiwa
kukusanya mayai ya samaki, akayarutubisha na kuyaangua kisha samaki hawa watoto
wakapelekwa kwenye matangi au mabwawa ya kufugia samaki. Mwanzoni ufugaji huu
ulifanyika kwenye maji baridi na samaki wa maji baridi na baadaye karne ya 20
hivi ufugaji wa maji-chumvi kwa kutumia samaki wa maji-chumvi ulianza kwa vile
ujuzi mpya ulikuwa umegunduliwa.
Historia ya ufugaji wa samaki
Tanzania haujawekwa vizuri kwenye maandishi, lakini kulingana na Balarin (1985)
anasema majaribio yalianza mnamo mwaka 1949 katika mikoa ya Tanga (Korogwe) na
Mwanza (Maly) ikionyesha kujengwa pia kwa mabwawa mengi ya samaki. Lakini
mabwawa haya yaliishia kutofanya kazi kwasababu ya kukosa usimamiaji mzuri,
matumizi ya technolojia isiyosahihi pamoja na matatizo mengine kama ya ukame na
miundo mbinu mibovu. Kulingana na ripoti iliyotolewa na FAO mwaka 1968
ilionyesha kuwa Tanzania ilikuwa na mabwawa 8000 ya kufugia samaki japo mengine
yalikuwa madogo yenye uzalishaji kidogo kulingana pengine na usimamizi mbovu.
Mwaka 1967 serikali ya Tanzania
ilianzisha kampeni ya kuhamasisha ufugaji wa samaki, lakini ilishindikana
kwasababu ya mipango mibovu na usimamizi mbovu. Mwaka 1972 kwa mara ya kwanza
ufugaji wa samaki ulipewa umuhimu kisera japo sheria ilitungwa mwaka 1970. Mwaka
1997 sera ya ufugaji wa samaki ilipitishwa iliyoipa kipaombele ufugaji wa
samaki.
Ufugaji wa samaki Tanzania kwa
sehemu kubwa unafanywa kama kazi ya ziada na wafugaji 17100 wanafanya ufugaji
wa maji baridi na 3 000 wa maji chumvi. Kuna takribani mabwawa 14100 yaliyo
maeneo mbalimbali ya nchi yetu na wafugaji wengi wa wale wafugaji wadogo wenye
mabwawa yenye ukubwa wa mita za mraba 150. Mgawanyo wa mabwawa katika nchi yetu
unategemea sana vitu vifuatavyo; upatikanaji wa maji, ardhi inayofaa kwa ufugaji
wa samaki, uelewa na uhamasikaji wa jamii ukitegemeana na umuhimu kiuchumi wa
ufugaji wa samaki. Kuna maeneo manne Tanzania ambako ufugaji wa samaki
umeshamiri kwa kiasi fulani (una mabwawa yanayozidi 1000), nayo ni Ruvuma (4942),
Iringa (3137), Mbeya (1176) na Kilimanjaro (1660). Mbali na kwamba kuna aina
nyingi sana za samaki wanaofugwa duniani, lakini katika nchi yetu ya Tanzania
ni aina kuu mbili zinazofugwa ambazo ni pelage au tilapia na kambale. Chaguo
hili la wafugaji wengi wa aina hizi limetokana na urahisi wa kuwafuga hawa
samaki kwa vile mahitaji yao si makubwa sana.
Kwa nini Mtanzania ufuge samaki?
Kuna upungufu mkubwa sana wa protini
duniani na hasa katika nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania inayotokana kwa
asilimia kubwa na vyakula vya aina ya nyama. Upungufu huu wa protini ambayo ni
muhimu kwa maendeleo ya kiafya ya binadamu hasa watoto wadogo na vijana wa umri
chini ya miaka 25 ambao wanahitaji kukuwa kwa haraka. Ugonjwa wa Kwashako kwa
watoto ndiyo matokeo ya upungufu wa protini mwilini.
Pia matumizi ya samaki na hasa
mafuta ya samaki ambayo ndo yanatumika sana kuwanywesha watoto wadogo
yamethibitika kisayansi kuwa yanasaidia sana ukuaji wa ubongo wa mwanadamu.
Lakini pia uwepo wa kiwango kidogo sana cha kolestero ambayo imeripotiwa
kusababisha ugonjwa wa moyo kimepelekea ongezeko la watu wanakula samaki.
Sababu zifuatazo hapa chini zinatoa
jibu la kwa nini Mtanzania ufuge samaki;
-Ongezeko kubwa la uhitaji wa samaki
ndani na nje ya nchi yetu kunakofanya samaki waliopa sasa kutotosheleza
mahitaji.
-Kupungua kwa samaki asili kwenye
mito, maziwa na bahari kunakotokana na uvuvi wa kupindukia na haramu.
-Urahisi wa kufuga samaki kwa vile
hawahitaji eneo kubwa na chakula kisichokuwa na gharama kubwa.
-Wanauwezo wa kutoa mazao
mengi(faida kubwa) katika eneo dogo tena ndani ya muda mfupi (uvunaji huanza
baada ya miezi mitatu au mine hivi na uvunaji wa mwisho kati ya miezi 6 hadi
12).
-Ufugaji wa samaki utasaidia familia
kupata kitoweo pasipo gharama za ziada na tena utapata protini ya uhakika.
-Upatikanaji wa maji maeneo mengi ya
nchi yetu hasa angalau kwa muda miezi michache kwa mwaka kiasi cha kutoa fursa
ya kuzalisha samaki katika kipindi ambacho maji yanakuwepo. Lakini pia maeneo
yenye maji ya bomba yanaweza kuzalisha samaki muda wote wowote.
-Samaki wanavumilia sana magonjwa,
hata mazingira duni wanauwezo wa kuishi
-Ardhi tuliyonayo maeneo mengi ya
Tanzania inakidhi ufugaji wa samaki
Tatizo la kuwa kuwa na ufugaji mdogo
wa samaki unachangiwa kwa kiasi kikubwa uduni wa elimu ya ufugaji wa samaki
katika maeneo mengi. Maeneo ambayo elimu ya kutosha imetolewa watu wengi
wamenufaika na ufugaji wa samaki na ufugaji umeshamiri kwa kiasi fulani. Ufugaji
wa samaki hauhitaji rasilimali nyingi au zilizo nje ya uwezo wa mwanchi wa
kawaida wa Tanzania. Mahitaji ya samaki mengi yanapatikana katika maeneo
anayoishi mwananchi na wala hauhitaji muda mwingi kiasi cha kuathiri kazi
nyingine.
Kama ilivyo kwa mifugo mingine
yeyote ile, kabla ya kuanza ufugaji kuna mambo muhimu yanayopaswa kuzingatiwa
ili ufugaji wako uweze kuwa na tija iliyokusudiwa. Mambo hayo ni kama
ifuatavyo:
1. Chagua mbegu bora ya samaki
unaotaka kuwafuga ili wakuletee mazao bora na mengi
2. Samaki wapewe makazi bora
yatakayo msitiri dhidi ya hali mbaya ya hewa kama joto, baridi n.k yaliyo safi
wakati wowote ili kuepusha magonjwa.
3. Hakikisha samaki wanapewa chakula
chenye viini lishe vinavyohitajika na kiwe cha kutosha ili waweze kukua na
kuzaliana kwa wingi na uwauze kwa wakati.
3. Hakikisha samaki wagonjwa
wanapewa tiba kwa wakati ili usisambae kwa wengine lakini pia yeye mwenyewe
asidhoofike na kufa.
4. Chagua eneo zuri linalofaa ufugaji
kwa kuangalia upatikanaji wa maji ya kutosha, aina ya udongo, mwinuko na liwe
karibu na nyumbani kwako.
5. Angalia uhitaji wa soko katika
eneo husika kama unapanga kufuga kibiashara
NAMNA YA KUANZA UFUGAJI
Ufugaji unaanza na utengenezaji wa
eneo la kufugia samaki yaani bwawa au tanki kutegemeana eneo ulilo nalo. Hapa
nitongelea mambo muhimu ya kuangalia kama unataka kufuga samaki kwenye bwawa na
mabwawa mengi nchini yale ya udongo. Mambo muhimu ya kuangalia wakati
unaangalia eneo la kujenga bwawa la samaki ni eneo la ardhi lilivyo, upatkanaji
wa maji na aina ya udongo.
1. Eneo la ardhi
Hakikisha eneo la ardhi ni tambalare
na mwinuko kidogo unaruhusiwa, lakini eneo hilo lisiruhusu kuwepo kwa mafuriko.
Ukubwa wa eneo utategemea na kiasi cha samaki unaotarajia kuwafuga. Hakikisha
kuwa eneo hilo halina aina yeyote ile ya uchafuzi wa mazingira, lisiwe na miti
mingi na vichaka vitakavyozuia jua na mwanga.
2. Upatikanaji wa maji
Maji ndo mazingira yanayomfanya
samaki aishi kwani upumuaji wake (kutumia matamvua) unategemea kwa asilimia 100
uwepo wa maji, nje ya maji hishi dakika kadhaa tu kabla ya kupoteza uhai
wake. Hivyo eneo la kufugia lazima liwe na maji ya kutosha na salama kwa
kipindi cha mwaka mzima. Vyanzo vya maji kwa ajili ya ufugaji wa samaki ni kama
chemichemi, mito, maziwa na maji ya ardhini (visima). Hakikisha vyanzo vya maji
ni salama kwa maana kuwa kusiwe na madawa yanayoweza kuathiri samaki mfano
madawa ya kupulizia nyanya au mbogamboga. Maji yaliyo ndani ya bwawa yanapaswa
kuwa na joto kwa kiasi fulani kwani ni muhimu sana kwa ukuaji wa samaki.
Tilapia anakuwa vizuri katika maji yenye uvuguvugu (nyuzi joto 25-30) katika
nyanda za chini lakini anaweza kuishi katika maji ya baridi sehemu za mwinuko
akikkua taratibu na kuzaliana polepole.
3. Aina ya udongo
Maeneo yenye udongo wa mfinyanzi
yanafaa sana kuchimba mabwawa ya kufugia samaki. Udongo mzuri unatakiwa usiwe
na changarawe, mawe wala usiwe na mchanga mwingi kwani hautakuwa na uwezo wa
kutuamisha maji kwa muda mrefu. Eneo lenye udongo kama ule unaotumika
kutengenezea vyungu na kufyatulia matofali ndo mzuri sana kwa kwa kujenga bwawa
la samaki.
4. Mambo mengine ya kuangalia wakati wa kuchagua eneo la
ujenzi wa bwawa
a)
Ukaribu na soko la samaki:
Bwawa
ni vema likajengwa karibu na soko la samaki lilipo la sivyo kuwepo na miundo
mbinu ya uhakika ya kuwafisha hao samaki sokoni bila kuharibika. Hasa hii
itakuwa muhimu sana endapo unakusudia kufanya ufugaji mkubwa na itapunguza
uharibikaji wa samaki wakati wa kuvua.
b)
Upatikanaji wa pembejeo:
Upatikanaji
wa vifaranga katika eneo la karibu ni vizuri ili kupunguza vifo vya mbegu hizo
za samaki wakati wa kusafirisha. Pembejeo nyingine ni pamoja na upatikanaji wa
mbolea (samadi na ya kiwandani) lazima vizingatiwe kwani ni muhimu kwa
urutubishaji wa bwawa wakati unatengeneza chakula cha samaki.
c)
Miundo mbinu:
Hakikisha
miundo mbinu ya mawasiliano inapatikana mfano simu, barabara, na umeme hasa
kama unakusudia kufanya ufugaji mkubwa. Hivi vitakusadia sana kujua soko na
kuwafikisha samaki sokoni kwa wakati wakati wanapohitajika.
d)
Wafanyakazi:
Ufugaji
mkubwa unahitaji msaada wa watu wengine wa kukusaidia kufanya kazi kwenye
shamba lako la samaki. Tumia watu wenye ujuzi wa kufuga samaki, wenye kujituma
kufanya kazi hiyo na ikiwezekana wapelekwe kozi ili wawe msaada mkubwa kwako na
kazi ifanywe kwa ustadi.
e)
Ushauri wa kiufundi:
Kama
wewe si mtaalamu na wakati mwingine kama ni mtaalamu hakikisha kwamba unauwezo
wa kupata ushauri pale utakapo hitaji. Ushauri unaweza kuupata toka kwa wafugaji
wenzako wa samaki au hata kwa maafisa wa samaki walipo katika eneo husika.
Lakini kwa utandawazi wa sasa ushauri unaweza kuupata toka hata kwa mtu aliye
mbali. Thibitisha ushauri unaopewa kwa watu zaidi ya mmoja ili kujiridhisha.
f)
Ushindani:
Ni vema kujua washindani wako katika
ufugaji na nguvu waliyonayo kibiashara katika eneo lako. Hii itakusaidia kujua
kama ufugaji wako utakuwa na manufaa kwako na hasa kama umekusudia uwe wa
kibiashara.
g)
Maswala ya Kisheria:
Ni vema kujiridhisha kama kunasheria inayozuia
kufanya ufugaji wa samaki katika eneo husika ili isije kukuletea matatizo
baadaye. Angalia sheria ya ufugaji wa samaki, sheria ya ardhi, sheria ya maji
na sheria ya mazingira zinasemaje juu ya ufugaji wa samaki katika eneo kama
hilo unalokusudia kufugia samaki.
Baada ya kujiridhisha na mambo yote
hapo juu sasa unaweza kuendelea na mipangilio ya ujenzi wa bwawa.
5. Aina ya mabwawa ya kufugia samaki
Mabwawa yote yanayotumika kufugia
samaki yanaangukia katika aina kuu tatu na uchaguzi wa aina ya bwawa lipi
litumike wapi inategemea sana mwonekano au sura ya ardhi litakapokuwa bwawa
hilo. Aina zenyewe kama ifuatavyo:
Mabwawa ya kukinga mto:
Mabwawa haya yanatengenezwa kwa kujenga
ukuta utakaowezesha maji kusimama kwa kukinga mto au kijito kwa ajili ya
ufugaji wa samaki. Mifereji ya kuchepusha mto hujengwa ili kuruhusu maji
yapungue pale yanapokuwa mengi na mengine huwekewa chujio sehemu ya kutolea
maji katika ule usawa unahitajika ili maji yakifika pale yatoke bila kutoka na
samaki.
Mabwawa haya
huchimbwa katika nchi yenye uwanda wa tambarale lakini yenye chemichemi za maji
yanayobubujika kutoka ardhini ili bwawa likichimbwa yaweze kujikusanya ndani ya
bwawa tayari kwa ufugaji wa samaki. Wakati wa kuvuna samaki si rahisi kuondoa
maji hadi ukingo wa bwawa ubomolewe ili kuruhusu maji yatoke.
Kuna maeneo ambayo ardhi yake ni ya mwinuko na hivyo mabwawa
ya aina hii hutumika kufugia samaki. Lakini pia aina hii ya mabwawa hujengwa
hata mahali ambapo si pa mteremko ila kwa chini sakafu yake huwa ya mwinuko.
Maji huingia na kutoka kwenye bwawa kwa njia ya mifereji au bomba. Na hii ndiyo
aina ya mabwawa inayotumika na watu wengi kufugia samaki.
6. Aina ya mifumo ya ufugaji samaki
Ipo mifumo ya aina mbili; ya maji
yaliyotuama ambao maji yakishajazwa ndani ya bwawa hukaa humo kwa muda mrefu
bila kutolewa na mfumo wa maji yanayotembea ambapo maji huruhusiwa kuingia na
kutoka bwawani wakati wote. Mfumo huu wa pili tofauti na wa kwanza mfugaji
hawezi kurutubisha bwawa kwani virutubisho vitachukuliwa na maji na hvivyo ni
wa gharama kubwa kwani unategemea chakula achowalisha samaki kila siku.
7. Aina ya samaki wanofugwa
Zipo aina nyingi sana za samaki
wanaofugwa duniani, lakini kwasabau ya urahisi wa kufuga na gharama kidogo za
ufugaji ambazo mfugaji wa kawaida anaweza kuzimudi, Tanzania kuna aina kuu
mbili tu zinazofugwa na watu wengi. Ambazo ni perege (tilapia) na kambare
(Catfish) ambao mahitaji yao si makubwa sana ukilinganisha na samaki
wengine.Perege yeye ni samaki wa maji moto lakini kwa asilimia kubwa anafugwa
kwenye maji baridi, kambare yeye pia anafugwa zaidi katika maji baridi.
Tatizo la ufugaji wa perege kwenye mabwawa ni uzalianaji usiodhibitika wakati changamoto ya ufugaji wa kambare ni vifo vingi hasa siku 14 za mwanzo mara baada ya kuanguliwa kwa mayai.
Tatizo la ufugaji wa perege kwenye mabwawa ni uzalianaji usiodhibitika wakati changamoto ya ufugaji wa kambare ni vifo vingi hasa siku 14 za mwanzo mara baada ya kuanguliwa kwa mayai.
No comments:
Post a Comment